NAMNA UNAVYOWEZA KUTUMIA NAFASI YA MLINZI KWENYE ULIMWENGU WA ROHO KUFANYA MAOMBI YENYE MATOKEO MAZURI (Sehemu ya 2)

Na: Patrick Sanga

Mada: Mambo muhimu kujua na kuzingatia kwa Mlinzi ili maombi yake yawe na mafanikio.

Shalom, katika sehemu ya kwanza tuliangalia tafsiri ya kuwa Mlinzi katika ulimwengu wa roho, ili kusoma sehemu hiyo tafadhali bonyeza link hii  https://sanga.wordpress.com/2017/07/05/namna-unavyoweza-kutumia-nafasi-ya-mlinzi-kwenye-ulimwengu-wa-roho-kufanya-maombi-yenye-matokeo-mazuri-zaidi-sehemu-ya-1/ Kuanzia sehemu hii ya pili kwa neema ya Mungu nitaanza kuandika kuhusu Mambo muhimu kujua na kuzingatia kwa Mlinzi ili maombi yake yawe na mafanikio. Naam fuatana nami tuendelee…

Jambo la kwanza: Jifunze kuutunza utakatifu wako

Biblia katika Mambo ya Walawi 20:26 inasema Nanyi mtakuwa watakatifu kwangu mimi; kwa kuwa mimi Bwana ni mtakatifu nami nimewatenga ninyi na mataifa, ili kwamba mwe wangu’. Pia katika 1Petro 1:15 imeandikwa ‘bali kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote; Zaidi katika Waefeso 5:8 imeandikwa ‘Kwa maana zamani ninyi mlikuwa giza, bali sasa mmekuwa nuru katika Bwana; enendeni kama watoto wa nuru’.

Kuwa mtakatifu ni kuishi au kuenenda katika utaratibu wa yeye aliyekuita alivyo. Mlinzi anapaswa aishi maisha ya kutojichafua kwa kujitenga na uovu, asiwe mtu wa maneno mengi na wala asimpe adui nafasi itakayomwondolea utakatifu wake ili kuruhusu mawasiliano mazuri kati yake na Mungu na maombi yake yaweze kujibiwa.

Katika Isaya 59:1-2 Biblia inasema ‘lakini maovu yenu yamewafarikisha ninyi na Mungu wenu, na dhambi zenu zimeuficha uso wake msiuone, hata hataki kusikia’. Katika Isaya 1:15 imeandikwa ‘Nanyi mkunjuapo mikono yenu, nitaficha macho yangu nisiwaone; naam, MWOMBAPO MAOMBI MENGI, sitasikia; mikono yenu imejaa damu’. Hii ni kutuonyesha kwamba dhambi ni chukizo kubwa mbele za Mungu kiasi cha kumfanya Mungu akatae kusikia na hivyo kujibu maombi (Yohana 9:31).

Mungu anajua kwamba ikiwa watu wake watajifunza kuishi kwa kuongozwa na Roho, agizo la utakatifu linatekelezeka (Wagalatia 5:16-17, 1Yohana 3:3-10), naam katika uaminifu wake BWANA hawezi kutoa maelekezo ambayo hayatekelezeki vinginevyo hakuna atakayemuona (Waebrania 12:14). Swali muhimu ni je kwa nini bado watoto wake wanatenda dhambi? – ni kwa sababu bado hawajamjua jinsi alivyo Mtakatifu, ndiyo maana imeandikwa ‘Kila akaaye ndani yake hatendi dhambi; kila atendaye dhambi hakumwona yeye, wala hakumtambua’ (1Yohana 3:6).

Hivyo lazima watoto wa Mungu wajilinde (kwa kutompa adui nafasi) na kujiepusha wasimtende Mungu wao dhambi, na mwovu hatawagusa (1Yohana 5:18), ikiwa wanataka kuona matokeo mazuri ya maombi yao. Hatuna sababu ya kuomba maombi mengi ambayo tunajua kwamba kwa mujibu wa neno la Mungu hayasikilizwi na hayatajibiwa, tunahitaji kuhakikisha muda wote tunaenenda kama wana wa nuru.

Rejea  Pigo la wana wa Haruni Nadabu na Abihu (Mambo ya Walawi 10:1-11). Katika kitabu cha Kutoka 19:12 imeandikwa Makuhani nao, wamkaribiao Bwana, na wajitakase, Bwana asije akawafurikia’ (Ona pia Isaya 52:11). Neno hili Bwana alilisema lakini watoto wa Haruni hawakulizingatia. Dhambi ya vijana hawa ilipelekea kifo chao wakiwa madhabahuni.

Hili linatufundisha kwamba hali ya muombaji ina nafasi kubwa sana katika kuamua matokeo ya maombi yake. Je, mwombaji anastahili na ujasiri wa kusimama na kuomba mbele za Mungu au la?. Kumbuka utakatifu unaruhusu mawasiliano kati yako na Mungu, wakati dhambi inakata mawasiliano husika. (1Yohana 3:21-22, Waebrania 4:16)

Hata hivyo pamoja na wana Haruni kufa walivyokuwa Haruni na wanawe waliosalia waliagizwa kutotoka nje ya hema ya kukutania na kwenda kushiriki maombolezo, ispokuwa ndugu zao. Hili linatufundisha kwamba haijalishi Mlinzi atakutana na changamoto gani, hatakiwi kuruhusu changamoto hizo zimuondoe kwenye nafasi yake na kuathiri wajibu wake tokana na umuhimu wa nafasi yake na upako ulio juu yake.

Mlinzi anapaswa kuwa mtu wa toba na kujitakasa akihakikisha anatunza mavazi yake yasichafuke (kuwa mtakatifu). Jambo hili litamsaidia kila aombapo ASIHUKUMIWE moyoni na hivyo kuwa na UJASIRI wa kusimama mbele za BWANA na kupata mpenyo unaostahili  kuwasilisha hoja za watu wake.

Somo litaendelea…

Utukufu na Heshima vina wewe Yesu, wastahili BWANA.

6 comments

Leave a comment