NAMNA MWANAMKE ANAVYOWEZA KUTUMIA NAFASI ZAKE KUBADILISHA MAISHA YA NDOA YAKE (Sehemu ya mwisho)

1

Na: Patrick Sanga

Heri ya ‘Christmas’ na mwaka mpya wa 2014

Salaam nyingi kupitia jina la BWANA wetu Yesu Kristo.

Naomba nianze kwa kumshukuru Mungu ambaye leo ameniwezesha kukamilisha sehemu ya mwisho ya ujumbe huu muhimu kwa uponyaji wa ndoa za watoto wake. Kimsingi haikuwa kazi rahisi lakini kwa msaada na uongozi wake, ujumbe huu mrefu umekamilika. Katika kumalizia sehemu hii ya mwisho nitaandika mambo manne (4) ambayo mwanamke anapswa kuyazingatia ili kubadilisha maisha ya ndoa yake kwa kutumia nafasi zake ambazo ni; mwanamke kama msaidizi, mshauri, mjenzi, mlinzi na mleta kibali. Mambo hayo ni pamoja na:

  • Ndoa ni wito wa mapungufu

Mama mmoja ambaye ndoa yake ilikuwa inasumbua alinitafuta na kuniambia, Mtumishi, changamoto za ndoa yangu ni kubwa kiasi kwamba sasa ni majuto tu, sina raha kabisa hata kidogo, nimekuwa mtu wa kuumizwa na kulia kila siku kwa sababu ya ndoa yangu, naomba msaada wako. Nilimsikiliza kwa kirefu katika yote aliyonieleza kwa upana wake.

Ukweli ni kwamba mpaka leo mama huyu simfahamu hata kwa sura, lakini BWANA alinijulisha kwamba ndani yake kuna huduma kubwa, ambayo Shetani anapamba nayo kupitia mumewe. Nilipojua nafasi ya huyu mama si tu kwa muewe bali kwa mwili wa Kristo kwa ujumla ilibidi kulipa kipaumbele suala lake mpaka Mungu aingile kati. Kwa kifupi nilianza taratibu kumfundisha jambo hili, nikamuonyesha nafasi zake na namna ya kuzitumia, naam naye akaweka kwenye matendo na sasa ndoa yake, BWANA ameiponya, wanaendelea vizuri kifamilia na kihuduma pia.

Jambo ambalo nimejifunza kupitia baadhi ya wanandoa ni kwamba, ndoa ni wito wa mapungufu. Unapoingia kwenye ndoa tegemea kukutana na changamoto kadhaa kutoka mwenza wako na hivyo kuwa tayari kuzikabili na kuvumilia. Kuna mapungufu ambayo yataisha kabisa kadri unavyoendelea kukaa kwenye nafasi zako na pia yapo ambayo hayataondoka kabisa kwa kuwa hayo ndiyo sababu ya wewe kuunganishwa na mwenzi wako, na Mungu aliona katika wanawake wengi wewe ndiye unayeweza kuchukuliana na kumsaidia katika mapungufu yake.

Wapo akina mama ambao wanatamani sana waume zao wabadilike tabia zao na zifanane na za kwao kabisa, napenda kukuambia kwamba hilo haliwezekani.  Naam, ile kwamba wewe ni mwanamke na yeye ni mwanaume ni dhahiri kwamba kuna vitu hamuwezi kufanana. Licha ya tofuti za kijinsia, malezi ambayo kila mmoja amepata kwenye famila yake, hitoria zenu, tofauti ya elimu zenu, vipato vyenu, umri wenu n.k. ni dhahiri kwamba mapungufu yatakuwa ni sehemu ya maisha kwenu. Sharti mjifunze kuchukuliana na kusameheana katika madhaifu na mapungufu hayo.

  • Tumia muda mwingi kuomba na si kuongea (Mithali 10:19,17:27, 18:21)

Maneno ni moja ya vyanzo vikubwa vinavyochangia kuharibu ndoa nyingi leo. Biblia katika kitabu cha Mitahli 10:19 inasema ‘Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na maovu; bali yeye azuiaye midomo yake hufanya akili’. Wapo baadhi ya akina mama ambao kueleza wengine mambo ya ndoa yao ni kawaida yao. Jambo baya zaidi ni kwamba wanawasema waume zao vibaya hata kwa watu ambao hawakustahili kuelezwa hayo. Kumbuka imeandikwa pia ‘Mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi, Na wao waupendao watakula matunda yake’ (Mithali 18:21)

Je unatumia muda kiasi gani kuomba kwa ajili ya mumeo? Na unatumia muda kiasi gani kuzungumza na watu wengine kwa siku? Naam nakushauri jifunze kutumia muda mwingi kuomba kwa ajili ya ndoa yako na kwa hakika BWANA Mungu atakufunulia mambo mengi sana kwa habari ya nyumba yako.

Biblia katika kitabu cha Ayubu 13:5 inasema “Laiti mngenyamaza kabisa, hilo lingekuwa hekima kwenu’. Sikia mwanamke, licha ya matendo, hekima kwa sehemu kubwa inadhihirika kwa njia ya kinywa, naam kunyamaza ni bora kuliko kunena, na hasa unapokuwa na hasira, chunga sana usinene maana hekima haifanyi kazi na hasira bali upole.

Katika Mithali 17:27) imeandikwa “azuiaye maneno yake ni mwenye maarifa; Na mwenye roho ya utulivu ana busara”. Hivyo nakushauri tumia muda wako mwingi kuomba kwa jili ya ndoa yako na si kuongea mambo yasiyojenga, ukijua kwamba maneno ni moja ya silaha kubwa ambayo Shetani anatumia kubomoa ndoa nying sana hata leo.

  • Usiwaze mabaya juu ya mume wako

    Nilipotembelea mkoa fulani kikazi, baba mmoja aliniomba nikazungumze na mke wake, ambaye aliamua kuondoka nyumbani kwa zaidi ya miezi sita na kwenda kuishi kwa wazazi wake. Baada ya kuzungumza na huyu baba kwa upana nilikubali na kisha nikapanga muda wa kuonana na mke wake. Tulipoonana alinieleza kile kilichomuumiza na kumpelekea kuondoka kwa mumewe. Katika kuzungumza kuna wakati yule mama alisema ‘natamani huyu mwanaume angekufa kabisa’.

    Binafsi nilifikiri amekosea nikamuuliza umesemaje? Akarudia tena kusema natamani afe naamini nitapata amani zaidi kwa maisha yangu yaliyosalia. Nilipomuuliza kwa nini unafikiri afe? akajibu yeye si mtu sahihi aliyepaswa kunioa, kwani walikuja wengi sana, kunichumbia, sijui kwa nini nilimkubali huyu na ndio maana leo naumia hivi.

    Nami nikamwoji je unajua athari ya hayo unayosema? Hujui kwamba akifa nje ya muda na mapenzi ya Mungu, damu yake itadaiwa mikononi mwako?  Kuwaza hivyo ni kukosea sana, tayari mlishafunga ndoa, na sasa unapaswa kufikiri namna ya kubadilisha maisha ya ndoa yako kuwa kwenye hali bora zaidi na si kuendelea kubomoa. Ndipo nikamwambia ‘kama hutazijua na kuzitumia nafasi ulizopewa na Mungu, kamwe amani haiwezi kuja kwenye ndoa yako’. Ilichukua miezi yule mama kuelewa na kurejea kwenye nafasi zake, lakini ashukuriwe Mungu naye alifanyia kazi na sasa amerudi kwa mumewe wanaendelea vema.

Sikia mwanamke unayesoma ujumbe huu, madaam ulikubali kuolewa, usimpe ibilisi nafasi kwa kuwaza mabaya juu ya mume wako, ukihoji, kwa nini nilikubali kuolewa na huyu baba, au kusema najuta kuolewa na huyu baba, au laiti wangekuwa wanabadilisha wanaume ningebadilisha haraka wa kwangu nk. Kumbuka kutengemaa kwa ndoa yako ni kufanikiwa kwa makusudi ya ufalme wa Mungu hapa duniani. Changamoto mnazozipitia kama wanandoa lengo lake ni kuwatoa kwenye nafasi yenu ya kufanya kile chenye kuujenga ufalme wa Mungu.

Hivyo haijalishi mume wako kakosea nini, wewe mtwike Mungu fadhaa zako zote, na uwe tayari kusamehe na kusahau, wala usiawaze mabaya juu yake, kwa kuwa kadri unavyowaza mabaya ndivyo unavyoiingiza ndoa yako kwenye uharibifu, ndivyo unavyoyaumba na kuyaita mabaya zaidi yaje kwenye ndoa.

  • Nafasi yako ni ya thamani sana kwa mumeo

    Katika kusoma kwangu Biblia na kufuatilia sana kuhusu nafasi ambazo Mungu amempa mwanamke, nimegundua kwamba nafasi ya mke kwa mume ni ya muhimu sana. Pengine kwa kiasi fulani inafanana na nafasi ya Kristo kwa kanisa, maana ikiwa katika ulimwengu wa roho mwanamke amepewa kuwa Msaidizi, Mshauri, Mlinzi, Mjenzi na Mleta kibali, je haya si sehemu tu ya majukumu ambayo Yesu anayo kwa kanisa lake kwa ujumla?

    Nafasi ulizopewa na Mungu katika ulimwengu wa roho, ni ishara kwamba kufanikiwa kwa kusudi la Mungu kupitia ndoa yenu kunategemea sana namna ambavyo mwanamke anazitumia nafasi zake. Naam zaidi kukubalika, kustawi na kufanikiwa kila mume wako atendalo kunategemea pia namna ambavyo wewe (mke) utazitumia nafasi zako. Hivyo kuchelea kwako kutumia vizuri nafasi zako ni kukwamisha kusudi la Mungu kwenye ndoa yako, familia yako, jamii yako na taifa lako.

Ukweli ni kwamba ‘Mume wako anakuhitaji sana hata kama maneno na matendo yake hayaonyeshi kwamba anakuhitaji”. Naam, mumeo anakuhitaji kuliko unavyofikiri, kadri wewe unavyokaa kwenye nafasi yako ndivyo unavyosaidia familia yako, kijiji chako, kanisa lako na taifa lako. Naam mume wako anahitaji sana upendo wako,kumbuka upendo ndio uliomsukuma Kristo aje afe kwa ajili yetu (Yohana 3:16), ingawa hata leo wapo watu wasiomwamini, wenye kumtukana lakini yeye bado anawapenda.  Upendo wa Kristo ndani yako ukukumbushe kusimama kwenye nafasi zako kwa ajili ya mumeo.

Naam bado ningeweza kuandika mambo mengine mengi zaidi, lakini fahamu jambo hili,  laiti mwanamke akisimama na kuzitumia nafasi zake vema, mabadiliko na uponyaji mkubwa kwenye ndoa yake ni matokeo halisi ya kutarajia. Nafasi hizi tano zinampa fursa mwanamke ya kuruhusu mawazo ya Mungu kupitia ndoa yake kutimia na kuzuia mawazo ya Ibilisi kupitia ndoa yake yasitimie. Naam nafasi ya mwanamke katika ndoa ndiyo inayoamua uzima au mauti ya ndoa yake, nafasi ndizo zinazoamua kufanikiwa au kufeli kwa ndoa yake.

Hivyo endapo utayaweka mafundisho haya kuanzia sehemu ya kwanza kwenye matendo si tu ndoa yako itaponywa, bali, maombi yenu yatasikilizwa, mume wako atapata kibali mbele za BWANA, naam atakuwa mume bora katika jamii na kufanikiwa katika kila atendalo. Mahusiano na mawasiliano mazuri yatakuwa sehemu ya maisha yenu na hivyo kurahisisha kutekelezwa kwa kusudi la Mungu. Ninapomalizia ujumbe huu muhimu nakushauri usijitazame kama mwanamke wa kawaida bali jifunze kujitazama kutoka kwenye nafasi zako kama Msaidizi, Mshauri, Mlinzi, Mjenzi na Mleta kibali, naam na maisha ya ndoa yako yatabadilika.

Mungu wangu akubariki na kuiponya kabisa ndoa yako, kupitia damu na jina la Yesu, amen.

 

Utukufu na heshima vina wewe Yesu! Wastahili BWANA wangu.

32 comments

  1. Mtumishi wa Mungu leo nimefurahi kukutana na somo hili kwani limenisaidia mimi pamoja na mke wangu na limezidi kutuimarisha.Bt nitachangia kidogo na kuuliza maswali kidogo!Ujuwe ndoa nyingi au asilimia nyingi wapendwa wameingia kwenye ndoa kwa kutokujua maana yake au kwa kutokuwa na subira yaani ile haraka,wengine kwa kutumia akili zao tu kuona kama wamepatia vile kumbe wamebugi!sasa unakuta ndoa nyingi mtu hajampata yule ambaye ametoka kwa GOD MWENYEWE.Je unadhani Mwanamke au Mwanaume ambaye amekurupuka tu yaani hajapata yule aliyewake ndoa hiyo hata wacmame kwenye nafac zao mambo yataenda?.Na kama hajatoka kwa Mungu inamaana c size yake?coz atakuwa hamtimizii kila hitaji lake kuanzia kimwili na kiroho.je masomo haya yanamsaada gani kwa wanandoa wa namna hii?C unajua kuishi na acyekuwa wa kwako ilivyomtihani?Huoni ndoa hiyo itakuwa maskani ya shetan?yaani no maelewano,no baraka,no kuishi yaani ni tabu mtindo mmoja!unawasaidiaje wanandoa hawa ili waje wauone uzima wa milele?Ni hayo tu kwa leo.

    Like

    • Hello Tumaini ahsante kwa sana kwa comment hii mchango wako na maswali yako pia. Nafikiri mtazamo wa swali lako umejielekeza zaidi kwa watu ambao tunaweza kusema wamekosea wakiwa wameokoka tayari kwa maana ya kwamba mume na mke wameoana baada ya kuokoka ila tatizo lao ni kuchukuana kwa mazoea bila kutafuta uongozi wa Mungu. Endapo swali lako linajikita hata kwa wale ambao hawajaokoka, kwa hao ufumbuzi ni rahisi kwa kuwa wote wanakuwa bado hawajamjua Mungu ipasavyo, hivyo kadri anavyowaita ndivyo anavyozidi kuwatengeneza na ujumbe huu unawafanya wajue nini wajibu wao wakiwa kwenye ndoa kama wana wa Mungu.
      Biblia katika 1Wakorinto 7:8, 26 inasema v8 “Lakini nawaambia wale wsiooa bado, na wajane, Ni heri wakae kama mimi nilivyo”.v26 “Basi naona hili kuwa ni jema, kwa ajili ya shida iliyopo, kwamba ni vema mtu akae kama alivyo”. Paulo kutokana na utumishi wake aliona changamoto zinazozikabili ndoa nyingi hata kupelekea watu kumuacha Mungu, kuacha huduma na kuharibu ‘future’ zao kwa sababu ya ndoa.
      Kuna njia tatu ya namna ambazo watu wanawapata wenzi wao; (a) Kundi la kwanza ni lile ambao wanaamua tu kuchukuana bila hata kufikiri kwamba Mungu anahusika katika suala hili (b) Kundi ambalo wanajua Mungu anahusika lakini hawampi nafasi ya kuwa mshauri kwenye hili (c) Kundi ambalo linatambua nafasi ya Mungu katika kuanzisha ndoa hadi kuimalisha na linampa yeye nafasi kuwaongoza kufanya maamuzi sahihi.
      Ndoa ambayo msingi wake haukumuhusisha Mungu maana yake wahusika walichagua njia yao (permissive will of Man) na si kile Mungu alikuwa amekusduia juu yao yaani (perfect will of God). Soma Warumi 1:28 Biblia inasema ‘Na kama walivyokataa kuwa na Mungu katika fahamu zao, Mungu aliwaacha wafuate akili zao zisizofaa,wayafanye yasiyowapasa’. Hivyo ni dhahiri kwamba kundi hilo litaendelea kuteseka au kuvuna kile lilichopanda kwa kuchagua.
      Hata hivyo pili kutokana na ukweli kwamba Mungu wetu ni wa rehema – Kupitia rehema zake kuna baadhi ya watu hata kama walikosea bado kuna neema yake ya kuwasiaida hasa anapoona kuna mmoja wao anatambua kwamba alifanya uamuzi ambao unamgharimu katika kufanya mapenzi ya Mungu. Hivyo Mungu hutoa tena fursa kwa huyu mwanandoa hata kama ni kwa maumivu, alitumikie kusudi lake na kuhaikisha kwamba ndoa yake haitamfanya aikose mbingu, kwa kuwa Mungu wetu ni wa rehema na hafurahi kifo cha mwenye dhambi, imeandikwa mimi ndimi Mungu niyafutaye makosa yako kwa ajili yangu mwenyewe, hivyo kwa mazingira haya bado ujumbe utawasaidia wanandoa wanaoangukia kwenye kundi hili.

      Like

  2. mtumishi asante kwa somo, nimekuta mwisho ila nimepata kitu naomba unifanyie msaada wa kunipostia post za nyuma zinisaidie zaid. asante na ubarikiwe.

    Like

  3. Hakika mtumishi Mungu akubariki sana,kwa kifupi ndoa yangu imepona kabisa kabisa ndio leo tu nimemaliza kusoma sehemu ya tano na kwa jinsi Mungu alivyoniongoza ukanipitisha katika shule hii hata kama ndoa yangu labda ilianza kuwa na ufa natangaza ushindi na mrejesho wake katika Jina la Yesu.Mungu akubariki sana Mtumishi.ila naomba namba yako nina jambo nawiwa kupata ushauri kutoka kwako jinsi ya kulishughulikia kiMungu.

    Like

  4. Nimeipendaaaa sana mada ya nafasi ya mwanamke ktk ndoa Mungu awabariki
    Naomba u nitumie kwenye email yangu

    Like

  5. Mungu akubariki sana mtumishi kwa mafundisho yako, hakika yakitendewa kazi ndoa nyingi zitapona na kusudi la Mungu litatimia. Nimefurahi sana kupata mafundisho haya, ingawa bado sijaingia kwenye ndoa lakini naamini pindi nitakapoingia kwenye ndoa, ndoa yangu itakuwa na amani kwa kusimama katika nafasi yangu kama mke. Mungu na anitendee sawasawa na kuomba kwangu na mapenzi yake. Barikiwa sana.

    Like

    • Ahsante kwa swali zuri, sitegemei kwamba unataka nikujibu hapa bali naamini unataka niandaae pia mfululizo wa somo kuhusu wajibu wa mwanaume. Kama nilivyoeleza kwenye sehemu ya kwanza ya somo hili, ujumbe huu wa akina mama sikuandika ilimradi tu ninaandika bali ni matokeo ya migogoro mingi ambayo akina mama walinishirikisha na katika kuwaombea ndipo nikapewa ujumbe huo. Hivyo naomba nipewe muda nitaandaa na mfululizo wa akina baba pia wakati ukifika, tuzidi kuombeana.

      Like

  6. Ahsante sanaaaana kwa masomo mazuri kiukweli nimejifunza meeeengi sana naamini Mungu atanisaidia ili niweze kuyafanyia kazi ipaswavyo… UBARIKIWE SAAANA MTUMISHI WA MUNGU..

    Like

Leave a comment