NAMNA MWANAMKE ANAVYOWEZA KUTUMIA NAFASI ZAKE KUBADILISHA MAISHA YA NDOA YAKE (Part 2)

May 20, 2012

Na: Patrick Sanga

Maada: Nafasi ya Msaidizi, Mshauri na Mleta kibali  

Ili kusoma sehemu ya kwanza bonyeza link hii http://sanga.wordpress.com/2012/03/01/namna-mwanamke-anavyoweza-kutumia-nafasi-zake-kubadilisha-maisha-ya-ndoa-yake/

Mpenzi msomaji, Mungu akubariki kwa kufuatilia mfululizo wa somo hili. Ni imani na maombi yangu kwamba masomo haya yatafanyika msaada kwenye maisha yako na ndoa yako kwa ujumla. Katika sehemu hii ya pili nitaandika kuhusu nafasi tatu ambazo ni nafasi ya Mwanamke kama Msaidizi, Mshauri na Mleta kibali.

Mwanamke kama Msaidizi

Mwanzo 2:18 ‘BWANA Mungu akasema, Si vema huyo mtu awe peke yake, nitamfanyia msaidizi wa kufanana naye’.  Ukisoma mstari huu katika toleo la GNB Biblia inasema ‘Then the LORD God said, “It is not good for the man to live alone. I will make a suitable companion to help him.” Biblia inatueleza kwamba Adam ndiye aliyetangulia kwanza kudhihirishwa kabla ya Mwanamke. Kabla ya Hawa kuletwa, Mungu alimpa Adam majukumu mengi ambayo alipaswa kuyatekeleza.

Katika kutekeleza majukumu yake Adam aliona kwamba amepungukiwa mwenza wa kufafanana naye na ndani yake akatamani angepata mtu wa kuwa naye karibu kwa kila afanyalo. Ukweli huu tunaupata tukisoma Mwanzo 2:20 kwamba ‘Adamu akawapa majina yao kila mnyama wa kufugwa, na ndege wa angani, na kila mnyama wa mwituni; lakini hakuonekana wa kumsaidia Adamu aliyefanana naye. Naam kutokana na upweke wa Adam ndipo Mungu akamfanya Hawa mkewe kama msaidizi. Kitendo cha Mungu kumfanya mwanamke kama msaidizi ni ishara kwamba Mungu alijua kuwa Adam hawezi kuwa na ufanisi mzuri katika kutekeleza majukumu (Kusudi) aliyopewa bila mwenza wa kufanana naye.

Maandiko yanasema kwamba ‘Maana mwanaume hakutoka katika mwanamke, bali mwanamke katika mwanaume. Wala mwanaume hakuumbwa kwa ajili ya mwanamke, bali mwanamke kwa ajili ya mwanaume’ (1Wakorinto 11:8-9).  Ile kwamba mwanamke aliumbwa kutoka kwa mwanaume na kwa ajili ya mwanaume ni kuonyesha kwamba wajibu au nafasi mojawapo ya mwanamke ni kuwa msaidizi wa mumewe. Hata hivyo neno msaidizi halipaswi kutafsiriwa vibaya na kuonyesha kwamba mwanamke hana thamani.

Mwanamke ni msaidizi wa mume katika kulitumikia kusudi la Mungu isipokuwa kinacho watofautisha ni utendaji wao tu. Mume hapaswi kumdharau mkewe wala mke kumdharau mumewe kwa kuwa mume si mume bila mke na mke si mke bila mume, wao ni mwili mmoja, kusudi lao ni moja na BWANA wao ni mmoja.   Maandiko yafuatayo yanaonyesha baadhi ya mambo ambayo mwanamke anapokuwa katika nafasi ya Msaidizi anapaswa kuyafanya;

Tito 2:4 inasema ‘Ili wawatie wanawake vijana akili, wawapende waume zao, na kuwapenda watoto wao, na kuwa wenye kiasi, kuwa safi, kufanya kazi nyumbani mwao, kuwa wema, kuwatii waume zao wenyewe; ili neno la Mungu lisitukanwe’.

1 Timotheo 5: 14 ‘Basi napenda wajane, ambao si wazee, waolewe, wazae watoto, wawe na madaraka ya nyumbani; ili wasimpe adui nafasi ya kulaumu’. Ukisoma pia katika 1 Wakorinto7:4a kwa habari ya tendo la ndoa Biblia inasema ‘Mke hana amri juu ya mwili wake…’ na mstari wa 5a unasema’ Msinyimane isipokuwa mmepatana kwa muda…, Naam hii ina maana kama mke ataweka amri kwa habari ya tendo la ndoa kwa mumewe ajue kabisa ameshindwa kumsaidia mumewe na kuna hatari ya kuanguka kwenye zinaa. Naam Mungu anataka akina mama walioko kwenye ndoa wajifunze kuwasaida waume zao wasiingie kwenye zinaa.

Naam hata sasa ni muhimu sana wewe mama ukajua Mungu amewaunganisha ili kufanya nini hapa duniani kwa ajili ya ufalme wake. Changamoto kubwa iliyipo leo ni kwamba wanandoa wengi wameingia kwenye ndoa kwa sababu ni desturi ya wanadamu kuoa na kuolewa. Wengi wameshindwa kuunganisaha suala la kuoa au kuolewa na kumtumikia Mungu kupitia ndoa yao. Mungu anapokuunganisha na mumeo maana yake anakupeleka kwenye wajibu wa kuwa msaidizi kwa mumeo. Naam hakikisha kwamba unafanyika msaada kwa mumeo kwa namna ambayo kile ambacho mnajua kwamba Mungu amewapa kukifanya hapa duniani kinafanikiwa. Zaidi unaweza soma Mithali 31:10-31 ili kuongeza ufahamu zaidi kuhusu nafasi ya mwanamke kama Msaidizi.

Mwanamke kama Mshauri

Katika hali ya kawaida watu wengi hutafsiri mshauri kuwa msiaidizi. Kwa kuzingatia dhana ya nafasi katika ulimwengu wa roho imenilazimu kutenganisha ili kukuonyesha umuhimu wa nafasi ya mwanamke kama Mshauri. Biblia katika Mithali 31:26 inasema ‘Hufumbua kinywa chake kwa hekima, Na sheria ya wema i katika ulimi wake’.

Naam andiko hili linatupa kujua kwamba Mke ndiye mshauri mkuu wa mumewe. Siri moja ya mwanamke kuwa mshauri mzuri ni kuwa na ufahamu wa kutosha wa neno la Mungu. Hivyo kama Mke hana hekima itokanayo na neno la Mungu kwa wingi ndani yake, hawezi kuwa mshauri mzuri. Ushauri unategemea nguvu za ufahamu alizonazo Mwanamke, kadri anavyokuwa na ufahamu wa kutosha wa neno ndivyo anavyokuwa kwenye nafasi ya kutoa ushauri bora kwa mumewe.

Biblia katika kitabu cha Mithali 8: 14-16 inasema ‘Shauri ni langu, na maarifa yaliyo sahihi; Mimi ni ufahamu na mimi nina nguvu. Kwa masada wangu wafalme humiliki, Na wakuu wanahukumu haki. Kwa msaada wangu wakuu hutawala, Na waungwana, naam, waamuzi wote wa dunia’. Fahamu kwamba hekima ndani yako mama itakupa maarifa na ufahamu wa kumshauri mumeo ili kufanya maamuzi sahihi katika kila atendalo. Hekima ni sawasawa na   shauri/maarifa/ufahamu/nguvu. Ukiona kiongozi yoyote anatawala/anaongoza watu vizuri ujue washauri wake wanamshauri vizuri au ujue ana wahsauri wazuri. Vivyo hivyo mwanaume anafanya kazi zake vema na kufanikiwa katika yale atendayo ujue nyuma yake kuna mwanamke mwenye nguvu za ufahamu anayemshauri vema.

Naam chanagmoto au matatizo mengi yaliyopo kwenye ndoa leo ni matokeo ya akina mama kukosa hekima itokanayo na neno la Mungu ya kuwashauri waume zao. Wengi wanategemea akili zao, au ushauri wa rafiki zao nk. katika kuangalia ndoa zao na mambo yao yaendaje. Kutegemea ushauri wa watu wengine bila wewe mwenyewe mama kutafuta hekima itokanyo na Mungu kwanza inaweza kukufikisha kupata ushauri wa kipepo kama ilivyomtokea Hawa pale Bustanini. Kumbuka Mshauri ni mtoa taarifa, mtoa pendekezo juu ya nini mume wake aweza fanya au kutofanya.

Mwanamke kama mleta kibali.

Hii ni nafasi ya ajabu sana ambayo Mungu amempa mwanamke. Mwanamke anapokuwa kwenye hii nafasi mambo matatu yanafanyika; 1) Mume anaingia kwenye ngazi ya kushirikishwa siri/mambo/majukumu mengi kutoka kwa BWANA. 2) Kukubalika kwa mume wake katika jamiii/kazi/kanisa nk kunaongezeka 3) Na mwisho maombi ya mume wake yanasikilizwa. Mambo haya yanathibitishwa na Biblia katika  Mithali 18:22 inayosema ‘Apataye mke apata kitu chema; Naye ajipatia kibali kwa BWANA’, pia   Mithali 31: 23 inayosema ‘Mume wake hujulikana malangoni; Aketipo pamoja na wazee wa nchi’

Zaidi kwa habari ya maombi ya mume kusikilizwa au kutokusikilizwa Biblia katika      1 Petro 3:7 inasema ‘Kadhalika ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu; na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe’. Naam hii ni ishara kwamba mke anaweza kusababisha maombi ya mumewe yakasikilizwa au yasisikilzwe. Unaweza ukafikiri hili andiko linawahusu akina baba pekee, lakini ukilitafakari kwa upana utagundua kwamba linawahusu akina mama pia ili wajue kwamba kuwa mke ni nafasi ambayo inaweza kuzuia maombi/baraka/majibu au kukwamisha mafanikio ya waume zao kama hawatukuwa makini katika kuwasaidia waume zao kuishi nao kwa akili.

Si wengi wanaojua kwamba kuna maombi mengi ya familia/waume zao hayajibiwi kwa sababu maombi ya mume ambaye ndiye kichwa hayasikilizwi na Mungu. Na chanzo cha kutokusikilizwa ni kuharibika kwa uhusiano kati ya mume na ‘mleta kibali’ wake yaani mke. Hivyo wewe mama mwenye ufahamu huu jifunze kwenda mbele za Mungu na kuomba toba kwa ajili ya mumeo mara kwa mara. Kwa sababu kuna vitu au maamuzi anayoweza kufanya nay eye akaona yuko sahihi lakini kumbe ni uamuzi ambao unajenga ukuta kati ya maombi yake na Mungu wako.

Hakikisha unasimama vema kwenye hii nafasi ili Mungu alete uponyaji kwa mume wako na maombi yake yaweze kusikilizwa. Naam simama kwenye nafasi yako ili kumjengea mazingira mazuri mumeo ya kuishi na wewe, ndivyo na maombi yake yatakavyosikilizwa, ndivyo atakavyopata kibali mbele za BWANA, naam atakuwa mume bora katika jamii na kufanikiwa katika kila atendalo.

Tamati endapo mwanamke atakaa vizuri kwenye nafasi hizi haijalishi mume wake ni mgumu kiasi gani, mama akizungumza kwa maana ya maonyo au ushauri lazima mwanaume asikilize au kufuata kile ambacho msaidizi, mlinzi, mleta kibali wake nk anamweleza, na kama akikataa uharibifu ni haki yake. Mungu ameweka sauti ndani ya mwanamke ambayo inaweza kuleta uponyaji kwa mumewe endapo mwanamke atakaa vizuri kwenye hizi nafasi.

Ubarikiwe, tutaendelea na sehemu ya tatu…

Asomaye na afahamu!

 

USIPOKUWA NA WAZO JIPYA HUWEZI KUTOKA MAHALI ULIPO

May 17, 2012

Na: Patrick Sanga

Mwaka 2010 nilikwenda Mbeya kwa mapumziko ya likizo na familia yangu. Wakati huo kuna mambo kadhaa nilikuwa nayapitia ambayo yalikuwa yakinipa shida rohoni mwangu na nilitamani kuvuka kutoka hapo na kwenda hatua nyingine bora ya mafanikio. Hivyo nikadumu kumwomba Mungu anifungulie mlango na kunipeleka hatua nyingine. Katika kuendelea kuomba na kutafakari neno la Mungu ndipo nikasikia sauti ndani yangu ikisema ‘usipokuwa na wazo jipya huwezi kutoka mahali ulipo’. Ingawa neno hili lilikuwa jibu kwangu, ilinichukua muda mrefu kuelewa Mungu alimaanisha nini. Ndipo nikaendelea kuomba na kujifunza kutoka kwenye Biblia kuhusu jambo hili pamoja na kusoma vitabu kadha wa kadha. Kwa sababu hii nimeona ni vema nikushirikishe uzoefu wangu ambao nina amini na wewe utakusaidia pia.

Nilijifunza kwamba maamuzi ya mtu ni matokeo ya mawazo yake, na matedo ya mtu ni matokeo ya mawazo anayowaza jumlisha maamuzi anayotekeleza. Naam hii ina maana kwamba, kumbe wazo au mawazo yana nafasi kubwa sana katika kubadilisha maisha ya mtu kwa kumtoa hatua moja na kumpeleka hatua nyingine. Ni muhimu ujifunze kutafuta mawazo mapya ili kubadili maisha yako kuwa bora zaidi ukikumbuka kwamba Mungu anakuwazia mawazo ya amani daima (Yeremia 29:11).

Wazo ni nini?
Wazo ni mpango, lengo, pendekezo, dhana au picha ambayo Mungu, Shetani huweka au kupanda ndani ya mtu (moyoni) ili mtu alifanyie kazi na hivyo kufanikisha makusudi ya ufalme wake hapa duniani. Kama umesoma mfululizo wa masomo yangu juu ya vita vya kiroho ambayo niliandika siku za nyuma nimeeleza kwa upana sana juu ya namna Mungu, Shetani kila mmoja anavyotumia mawazo kuhakikisha makusudi yao yanafanikiwa hapa duniani, na hivyo kufanya vita vya kiroho kuwa vita ya mawazo.

Ukisoma Biblia utagundua kuna vyanzo vitatu vya mawazo navyo ni; kuna mawazo kutoka kwa Mungu (Yeremia 29:11), kuna mawazo kutoka kwa Shetani (2 Wakorinto 4:4) na pia kuna mawazo kutoka kwa mtu au watu (Isaya 65:2). Mwanadamu anapita katika hatua mbalimbali za maisha kama misiba, njaa, magonjwa, dhiki, kushindwa kufikia malengo, hali ngumu kiuchumi nk. Ni furaha sana kwenye ufalme wa giza kuona watoto wa Mungu wanaishi maisha ambayo Mungu hakuwapangia, namaanisha maisha ambayo mtu anaishi nje ya mawazo ya Mungu juu yake. Naam hii ndio kazi anayokazana kuifanya Shetani ya kuwafarakanisha watu na Mungu wao.

Zifuatazo ni hatua zitakazokusaidia kupata wazo jipya la kukutoa katika hali ya maisha ambayo wewe binafsi huridhiki nayo na kukupeleka kwenye eneo bora zaidi kimafanikio;

Hatua ya kwanza – Ni muhimu kujua mahali ulipo sasa
Hili ndio jambo la msingi kabisa la kuanza nalo ili kupata wazo jipya. Kimsingi unatakiwa kujua hali yako ya sasa ya kiroho, kifamilia, kihuduma, kiuchumi, kibiashara, kifamilia, kimahusiano nk. ikoje au ni ya namna gani? Je unaridhika nayo au la? kwa nini huridhiki nayo nk. Hali yako ya sasa ni matokeo ya kuwaza kwako juu ya hilo eneo. Kwa hiyo licha ya kujua mahali ulipo jiulize ni wazo au mawazo gani ambayo yalikufikisha mahali ulipo. Kwa kugha nyingine jiulize kwa nini upo ulivyo?
Yawezekana upo ulipo kwa sababu kuna mawazo fulani yaliingia moyoni mwako nawe ukayatafakari na kisha kuyafanyia kazi na ndio maana umefika mahali ulipo. Kumbuka maisha ya mtu ni matokeo ya mawazo na maamuzi anayotekeleza maishani mwake. Mfano; kutokutoa zaka na sadaka kwa uaminifu (Malaki 3:7-10), kukosa uaminifu, uongo au kumpa ibilisi nafasi nk ni vyanzo vya laana kwenye maisha ya mtu.

Hatua ya pili – Fahamu mahali unapotakiwa au unapotaka kwenda.
Kama huridhiki na hali yako ya sasa ya maisha, hii ina maanisha kuna hali nyingine bora zaidi ambayo unatamani kuifikia. Kwa sababu hii unahitaji kuanza kufikiri au kuwaza ni wapi unataka kwenda/kufika kwa maana ya mafanikio, ni hatua gani ya mafanikio kiroho, kihuduma, kifamilia, kibiashara nk unataka kuifikia maishani mwako? Naam unatakiwa kutoridhika na mazingira uliyonayo ili kuweka kiu ya wazo la kukutoa mahali ulipo.

Hatua ya tatu – Tumia Biblia kama msingi wa kupata mawazo/wazo jipya
Biblia inasema katika Yeremia 29:11 ‘Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema BWANA, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho’. Ni muhimu ukafahamu kwamba neno la Mungu ni jumla ya mawazo ya Mungu juu ya namna gani watoto wake wanapaswa kuishi ili kufanikisha maisha yao na kusudi lake hapa duaniani.
Biblia imejaa mawazo mapya toka kwa Mungu (Mithali 16:20, Joshua 1:8, Mithali 20:5). Naam bila kuwa na wazo jipya huwezi kutoka mahali ulipo. Soma kwa kulitafakari neno la Mungu, ndivyo utakavyojua kwa hakika Mungu anakuwazia mawazo ya amani kwenye kila eneo la maisha yako kuliko ulivyokuwa unafikiri.

Hatua ya nne – Jifunze kuwa na muda wa kuwaza
Hili ni jambo ambalo Shetani amefanikiwa kuwafunga watu wengi sana wasiliweke kwenye matendo. Mungu amemuumba mtu kwa namna ambayo kama mtu atakuwa na nidhamu ya kutenga muda kwa ajili ya kuwaza kile ambacho Mungu anaweka kwenye moyo wa mtu, basi maisha ya mwanadamu yangekuwa bora sana licha ya changamoto nyingi zinazomkabili.

Ni muhimu sana kwako kama mtoto wa Mungu kuwa na muda wa KUWAZA. Tafadhali nieleweke vema sijasema muda wa kuomba au kusoma neno, bali muda wa KUWAZA/KUFIKIRI kile Mungu anataka ukifanye hapa duniani kupitia mawazo anayotelemsha moyoni mwako. Jijengee nidhamu hii utaona mabadiliko makubwa sana kwenye kila eneo la maisha yako, anza hata kuwa na dakika kumi na tano, nusu saa, saa moja nk. (Zaburi1:1-2)

Hatua ya tano – Jifunze kufikiri kwa nyakati au ki-muda (1 Nyakati 12:32, Kumbukumbu 32:29, Luka 19:41-45).
Biblia iko wazi katika kitabu cha Mhubiri 3:1 ikisema ‘Kwa kila jambo kuna majira yake, na wakati wa kila kusudi chini ya mbingu’. Hii ina maana kila kusudi ambalo mwanadamu amepewa limefungwa kwenye muda na hivyo mwanadamu lazima ajifunze kushirikiana na kuukomboa muda/wakati (Waefeso 5:16) ili maisha yake binafsi yawe na mafanikio lakini pia kusudi la BWANA.
Hivyo tunajifunza kwamba kwa mujibu wa (Mhubiri 3: 1) ili mwanadamu aweze kushirikiana vema na muda, ni lazima ndani yake ajifunze kufikiri ki- muda (thinking in terms of time). Naam kila wazo au kusudi linalokuja moyoni mwake toka kwa Mungu, basi mosi atafute kujua muda wa hilo wazo kutimia ni lini , na pili ajifunze kuweka muda kwa kila mikakati au mipango ambayo anaiweka kwa ajili ya kutekeleza wazo husika. Mfano: Ni imani yangu kwamba Nuhu alipoambiwa tengeneza Safina, ndani yake alipiga mahesbu ya muda unaohitajika kwa ujumla na hivyo kila hatua ya ujenzi akaiwekea muda mpka Safina ilipokamilika.

Naam unahitaji wazo jipya kutoka kwa Mungu ili kutoka mahali ulipo kiroho, kiuchumi, kibiashara nk. Tafuta wazo jipya toka kwa Mungu, naam Kwa mapato yako yote jipatie ufahamu (Mithali 4:7)

Neema ya Kristo iwe nawe daima

THAMANI YA KIFO CHA YESU PALE MSALABANI

April 7, 2012

Na: Patrick Sanga

Heri ya pasaka mpenzi msomaji. Ni jambo la pekee tena kwa Mungu kutufikisha katika maadhimisho ya kumbukumbu za kifo chake na kufufuka kwake yaani pasaka. Kwa kifupi nimeona niandike ujumbe huu ili kukumbushana mambo muhimu kwa habari ya Pasaka.

Ni muhimu sana kukumbuka kwamba Yesu alikufa pale msalabani kwa sababu kubwa mbili moja ni ili kurejesha mahusiano ya Mungu na mtu kwa lengo la kumsaidia mtu aishi hapa duniani kwa kusudi la Mungu na pili ili tupate wokovu na kisha kuurithi uzima wa milele.

Biblia katika kitabu cha Mathayo 26:53-54 inasema ‘Ama wadhani ya kuwa mimi siwezi kumsihi Baba yangu, naye ataniletea sasa hivi zaidi ya majeshi kumi na mawili ya malaika? Yatatimizwaje basi maandiko, ya kwamba hivyo ndivyo vilivyopasa kujiri?’ Kutokana na andiko hili ni vema tukajifunza kwamba;

  • Upendo wake (Yesu) ndio uliomsukuma kuyatoa maisha yake kwa ajili yetu
  • Yesu alikuwa na uwezo wa kuangamiza askari waliokuja kumkamata, lakini hakufanya hivyo ili andiko/kusudi la Mungu lipate kutimizwa.
  • Ndani ya ufahamu wa Bwana Yesu kulikuwa na mwanadamu, ndio maana kwa kuangalia ‘future’ ya mwanadamu na kusudi la uumbaji wa Mungu ilimlazimu kupitia njia ngumu ya msalaba ili atupate mimi na wewe.

Naam ndugu zangu tujiulize, ni upendo wa namna gani wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake. Biblia inasema katika kitabu cha Waebrania 2:1-3 Kwa hiyo imetupasa kuyaangalia zaidi hayo yaliyosikiwa tusije tukayakosa. Kwa maana ikiwa lile lililonenwa na malaika lilikuwa imara, na kila kosa na uasi ulipata ujira wa haki, sisi je! Tutapataje kupona, tusipojali wakovu mkuu namna hii? Ambao kwanza ulinenwa na Bwana, kisha ukathibitika kwetu na wale waliosikia’

Katika kuendelea kuonyesha thamani ya kifo cha Yesu pale msalabani Yohana naye aliandika akasema ‘Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata  akamtoa Mwanawe pekee, ila kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye’ Yohana 3:16-17.

Jambo la muhimu ni kwamba Bwana Yesu hayuko kaburini tena, naam alikufa na kufufuka ili awalete wengi kwenye ufalme wake. Hivyo basi mpenzi msomaji nakusihi usiichezee neema hii, nakusihi usomapo ujumbe huu wewe ambaye hujaokoka, fanya maamuzi ya kuokoka na wewe unayemjua Mungu maanisha katika wokovu wako.

Twaliabudu na kulisifu jina lako wewe uliyeutoa uhai wako kwa ajili yetu ee Bwana.

Ahsante kwa siku njema ya leo ambayo Bwana umeifanya kwa ajili yetu ee Mungu.

Basi ndugu zangu tunapoadhimisha sherehe hizi za pasaka tusiifanye kazi ya Yesu pale msalabani kuwa ni bure, bali kuanzia sasa tusienende kama wamataifa waendavyo bali kama wana wa nuru.

Familia yangu pamoja nami tunawatakia heri ya pasaka, ‘Bwana Mungu awabarikie na kuwalinda’.

NAMNA MWANAMKE ANAVYOWEZA KUTUMIA NAFASI ZAKE KUBADILISHA MAISHA YA NDOA YAKE

March 1, 2012

Na: Patrick Sanga

Mithali 14: 1 ‘Kila mwanamke aliye na hekima hujenga nyumba yake; Bali aliye mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe’.

Mchungaji mmoja rafiki yangu aliniambia asilimia hamsini mpaka sabini ya changamoto au matatizo anayoshughulika nayo mara kwa mara katika kanisa lake ni ya wanandoa. Kwa lugha nyepesi asilimia 50 – 70 ni matatizo yatokanayo au yanayohusiana na ndoa. Binafsi pia kwa upande wangu kupitia nafasi yangu katika mwili wa Kristo, email za wasomaji ninazopata na pia baadhi ya semina za ndoa ambazo nimefanya kuhusu eneo hili nimegundua kwa hakika ndoa nyingi za wana wa Mungu zina shida na wao hawajajua kwamba vita hii inatoka kwa Shetani, maana anajua ndoa zikitengamaa ni faida kwa ufalme wa Mungu na ni uharibifu kwenye ufalme wake wa giza. Naam anapigana usiku na mchana ili kuhakikisha ndoa hazitengamai kwa kuleta fujo za kila aina.

Kila siku katika ndoa kuna changamoto zinazaliwa mpaka imefika mahala baadhi ya wanandoa wanawaza kwa nini walikubali kuoa au kuolewa. Kwa hakika laiti Biblia ingetoa mwanya kwa wanandoa kuachana basi kuna baadhi ya wanandoa wangehakikisha wanaitumia hiyo nafasi vizuri kwa kuwa ndoa zimegeuka ndoano. Matarajio ambayo kila mmoja alikuwa nayo kwenye ndoa anaona hayatimii. Kinachosumbua watu wengi ni kwamba kabla hawajaonana hawakujua nini kinakuja kupitia ndoa, hawakuweza kuona uhalisia wa maisha ya ndoa utakuwaje? Bali kila mmoja alikuwa na mtazamo/fikra na matarajio yake binafsi juu ya ndoa yake.

Naam zipo sababu nyingi sana zinazopelekea matatizo au changamoto kwa wanandoa. Katika somo hili nitaandika zaidi zile zinazotokana na upinzani kutoka kwa Shetani ili kuathiri kusudi la Mungu. Lengo la ujumbe huu ni kukufundisha wewe mama (Mwanandoa) namna ya kuzitumia ‘nafasi’ ambazo Mungu amekupa Kibiblia ili kuiponya ndoa yako au kubadilisha hali ya sasa ya ndoa yako endapo unaona si ile ambayo Mungu amekusudia.

Kwa nini Mwanamke?

Pengine utaniuliza kwa nini mwanamke ndiye awajibike katika kuponya au kubadilisha maisha ya ndoa yake? Binafsi katika kuisoma Biblia nimegundua kwamba kwa kuzingatia nafasi ambazo mwanamke amepewa kibiblia ni ishara ya kwamba kwa habari ya  ndoa, Mwanamke ana nafasi kubwa ya kuijenga au kuibomoa ndoa yake na hivyo nyumba yake kwa ujumla. Mara kwa mara Mungu ananifundisha masuala ya wanawake, suala la wanawake kuwa kwenye ‘nafasi zao’ husisitizwa sana.

Kwa nini nafasi?

Sijui kama unafahamu maana ya nafasi ambayo Mungu anampa mtu katika ulimwengu wa roho. Hizi ni nafasi ambazo Mungu amekupa wewe mawanamke katika ulimwengu wa roho ili uzitumie kufanikisha kusudi lake kupitia ndoa yako. Nafasi (position) ni eneo ambalo mtu anapaswa kuwepo kwa kuhusianisha na vitu au watu wengine, naam ni wadhifa ambao mtu anakuwa nao kwa kuhusianisha na mtu au watu wengine.

Kwa hiyo hizi ni nafasi ambazo Mungu amempa mwanamke zikihusiana na mwanaume katika kilitumika kusudi la Mungu hapa duniani. Mwanamke anapokuwa amesimama katika nafasi zake ndipo anapoweza kuruhusu mawazo ya Mungu kupitia ndoa yake kutimia naam ndivyo anavyoweza kuzuia mawazo ya Iblisi kupitia ndoa yake yasitimie. Naam nafasi ya mwanamke katika ndoa ndiyo inayoamua uzima au mauti ya ndoa yake, nafasi ndiyo inayopelekea kufanikiwa au kufeli kwa ndoa yake, nafasi ya mwanamke katika ndoa ndio inayoamua nini kingie au kitoke kwenye ndoa.

Katika kusoma kwangu Biblia nimegundua kwamba Mungu amempa nafasi zifuatazo mwanamke;

  • Mwanamke kama ‘msaidizi’ wa mumewe
  • Mwanamke kama ‘mlinzi’ wa mwanaume
  • Mwanamke kama ‘mjenzi’ wa nyumba yake
  • Mwanamke kama ‘mshauri’ wa mumewe
  • Mwanamke kama ‘mleta kibali’ kwa mumewe

Naam kutokana na changamoto zinazoendelea katika ndoa mbalimbali nimelazimika kuanza kuandaa mfululizo huu wa namna mwanamke anavyoweza kusimama kwenye nafasi zake na kuiponya ndoa yake. Jukumu langu kubwa itakuwa ni kufafanua kila nafasi ambayo mwanamke amepewa na namna anavyoweza kuitumia hiyo nafasi kubadilisha ndoa yake ambayo anaona inaangamia.

Somo litaendelea, maombi yako ni muhimu sana.

IJUE NA KUITUMIA NAFASI YAKO KAMA MLINZI KWENYE ULIMWENGU WA ROHO (Part 3)

February 3, 2012

(Umuhimu wa taarifa na mahusiano mazuri baina ya mlinzi na watu wa eneo lake)

Na: Patrick Sanga

Ili kusoma sehemu ya pili bonyeza link hii http://sanga.wordpress.com/2011/12/07/ijue-na-kuitumia-nafasi-yako-kama-mlinzi-kwenye-ulimwengu-wa-roho-part-2/

Katika sehemu ya pili naliahidi kwamba ningeanza kuelezea kuhusu nafasi mbalimbali za ulinzi, lakini ndani yangu nimesikia kuandika mambo kadhaa yafuatayo tena kabla sijaanza kuandika kwa habari ya nafasi husika. Ni imani yangu kwamba sehemu ya nne itaanza kwa kuelezea nafasi husika, fuatana nami tuendeleae.

Jambo ambalo nimesukumwa niandike kwa habari ya eneo hili la tatu ni umuhimu wa taarifa na mahusiano mazuri baina ya mlinzi na watu wa eneo lake.

Jambo la kwaza – Umuhimu wa taarifa ya mlinzi kwa watu wa eneo lake

Hebu tuangalie jambo hili kupitia kitabu cha Mathayo 25:1-13. Hii ni habari ya wanawali kumi waliokuwa wakimsubiri Bwana Harusi. Biblia inatuambia watano kati yao walikuwa na busara na watano walikuwa wapumbavu. Busara ya wale watano wa kwanza ni kuwa na taa zenye mafuta ya akiba huku wakimsubiri Bwana, na upumbavu wa wale watano wengine ni kuwa na taa zisizo na mafuta ya akiba huku wakimngoja Bwana harusi pia.

Kwa sababu ya Bwana harusi kuchelewa wanawali hawa wote waliamua kulala. Ule mstari wa sita na saba inasema ‘Lakini usiku wa manane, pakawa na kelele, Haya, Bwana arusi; tokeni mwende kumlaki. Mara wakaondoka wanawali wale wote, wakazitengeneza taa zao’.

Katika sehemu ya pili ya somo hili niliandika kwamba jifunze kuitazama taarifa ya mlinzi kama fursa ya matengenezo. Biblia iko wazi kwamba wanawali hawa waliamua kulala baada ya kuona Bwana harusi wao amechelewa. Kumbuka kwamba lengo la wote hawa ilikuwa ni kumlaki Bwana Harusi. Sasa kilichowaamsha toka usingizini ni ‘kelele za taarifa’ ambazo ninaamini zilikuwa za walinzi ambao jukumu lao ilikuwa ni kutoa taarifa juu ya uwepo au ujio wa Bwana harusi husika.

Kutokana na mfano huu tunajifunza kwamba mosi taarifa ya mlinzi/walinzi iliwasaidia wanawali kuamka kutoka usingizini maana walikuwa wamelala. Licha ya taarifa kuwasiaida kuamka usingizini, taarifa ya mlinzi ilitoa fursa ya wanawali kujiandaa. Tumeona katika mstari wa saba kwamba punde baada ya taarifa wale wanawali wakaamka na kuziandaa/zitengeneza taa zao. Naam taarifa ya walinzi ilitoa fursa ya matengenezo. Hivyo hata sasa Mungu anapoleta taarifa kwako, ujue analeta taarifa ya matengenezo, naam mbele kuna jambo linakuja, hivyo analeta taarifa mapema kupitia walinzi wako au wa eneo lako ili uitumie kutenda yapasayo. 

Jambo la pili – Umuhimu wa kuwa na mahusiano mazuri kati ya Mlinzi na watu wa eneo lake.

Kupitia mfano huu wa wanawali kumi tunagundua pia kwamba, taarifa ya mlinzi ilitoa fursa ya mawasiliano baina yao. Kabla ya taarifa hatuoni wanawali hawa wakiwasiliana kwa jambo lolote. Si hivyo bali pia tunagundua kwamba baada ya taarifa ya mlinzi ndipo fahamu za wale wanawali wapumbavu zikafunguka na wakajua mafuta yao hayatoshelezi. Kwa mujibu wa Biblia harusini aliruhusiwa kuingia mtu (mwanamwali) mwenye taa inayowaka yaani taa yenye mafuta.

Je, ni kwa nini wale wanawali wapumbavu kabla hawajaenda kulala hawakufikiri kwamba mafuta haya yakiisha na hatuna ya akiba hatuwezi kuingia harusini?  Huenda hawakujua kwamba mwanamwali mwenye taa inayowaka ndiye atakayeruhusiwa kuingia harusini. Jambo ninalotaka ulione ni kwamba pamoja na kutokujua kwao, walinzi wa mji walijua nini kinatakiwa kwa mtu kuingia harusini. Laiti wanawali wangekuwa na mahusiano mazuri na walinzi wa mji wangepewa siri kuhusu ujio wa Bwana harusi wao. Lakini kwa sababu hawakuwa na mahusiano mazuri na walinzi, walishindwa kuwauliza wale walinzi mahitaji ya msingi atakapokuaja Bwana harusi. Naam wakajikuta wameachwa na Bwana wao walipoenda kutafuta mafuta. 

Ukweli huu kuhusu mahusiano unathibitishwa katika kitabu cha Wimbo Ulio Bora 3:3 unaosema ‘Walinzi wazungukao mjini waliniona; Je! Mmemwona mpendwa wa nafsi yangu’. Habari hii inatueleza habari za kijana aliyekuwa anamtafuta mwenza (mpenzi) wake kwa muda mrefu bila mafanikio. Katika kuendelea kumtafuta ndipo akakutana na walinzi wa mji, akawauliza mmemwona mpendwa wa nafsi yangu?          Ni imani yangu walinzi wale walimjibu, kwa sababu mstari wa nne unatumabia ‘kitambo kidogo tu nikishakuwaondokea, nikamwona mpendwa wa nafsi yangu, Nikamshika nisimwache tena…’ Hivyo ufumbuzi wa tatizo (hitaji) la huyu kijana ulipatikana kwa walinzi wa mji. Kwa hakika mahusiano mazuri ya Walinzi na yule kijana yalipelekea hitaji la kijana kufanikiwa au kufikiwa.

Kutokana na habari hii ni dhahiri kwamba walinzi wamewekwa kwenye nafasi zao ili kuleta ufumbuzi juu ya changamoto zinazomkabili mwanadamu kwa kumjulisha mawazo ya Mungu juu yake, ili pia kumsaidia mwanandamu aishi kwa kulitumikia shauri la Mungu katika siku zake. Biblia katika kitabu cha Isaya 62:6-7 inasema  ‘Nimeweka walinzi juu ya kuta zako, Eee Yerusalemu; hawatanyamaza mchana wala usiku; ninyi wenye kumkumbusha BWANA, msiwe na kimya; wala msimwache akae kimya, mpaka atakapoufanya imara Yerusalemu, na kuufanya kuwa sifa duniani’.

Mungu anataka yawepo mawasiliano na mahusiano mazuri kati ya Mlinzi (Walinzi) na wanaolindwa. Katika andiko hilo hapo juu, licha ya Mungu kuweka walinzi juu ya kuta za Yerusalemu ilibidi awape taarifa na wakazi wa mji huo, ili wasije, walinzi hao wakatoa taarifa ya kile Mungu amesema na wakazi wa Yesrusalemu wakapuuza, mwisho wao wakaangamia.

Ukisoma pia Biblia katika kitabu cha Mathayo 24:43 inasema ‘Lakini fahamuni neno hili; kama mwenye nyumba angalijua ile zamu mwivi atakayokuja, anagalikesha, wala asingeliacha nyumba yake kuvunjwa’. Naam kiroho milinzi au walinzi ndio waliopewa uwezo wa kuona nini kinakuja juu yako, ndoa yako, kazi yako, huduma yako, taifa lako nk. Kwa sababu hii ni muhimu sana kuwa na mahusiano mazuri na mlinzi au walinzi ambao Bwana Mungu amekuweka chini ya Mlango au Himaya yao. Naam kufanikiwa kwa kazi ya mlinzi katika nafasi yake kunategemea mahusiano na ushirikiano anaopata kutoka kwa watu wa eneo lake.   

Mungu akubariki kwa kufuatilia mfululizo huu, usiache kuombea muendelezo wa somo hili. Tutaendelea na sehemu ya nne…

 

 

 

Follow

Get every new post delivered to your Inbox.